Академический Документы
Профессиональный Документы
Культура Документы
II MATIBABU
Kwa toleo hili la ki-swahili tunamshukuru Emmanuel Biligeya kwa kazi yake ya utafsiri na
Mchg Hezron Shimba na Maike Ettling kwa kuhariri. Pia tunaishukuru HUYAMU (Idara ya
Afya ya AICT – Dayosisi ya Mara & Ukerewe) kwa ushirikiano wao wa karibu.
Anamed ingependa taarifa zilizo katika kijitabu hiki zisambazwe mahali popote zinapowezekana
kufika. Tunawahamasisha watumiaji wa kitabu hiki kukitafsiri katika lugha zao. Hata hivyo kwa
kuwa mambo yaliyomo yanaboreshwa mara kwa mara, tafadhali wasiliana na anamed kwanza.
Haki miliki ya tafsiri zote inabaki na anamed. Hakuna sehemu ya kitabu hiki inayoruhusiwa
kuchapwa na kuuzwa tena.
Mabango ya rangi (anamed No. 403) vinaonyesha mimea iliyoelezwa katika kitabu hiki.
Toleo la pili la kitabu hiki linapatikana katika lugha ya kifaransa, kireno, kijaluo, kiamharic,
kiateso na kichichewa. Baadhi ya vitabu vya anamed vinapatikana katika baadhi ya nchi za
Afrika.
Wafuatao wanaunganisha anamed na ndio wauzaji na wasambazaji wa vitabu na vifaa vya
anamed:
anamed, Schafweide 77, D – 71364 Winnenden, Germany
Email: anamedhmh@yahoo.de
Website: www.anamed.net
YALIYOMO
anamed inafanikisha lengo hili kwa kuwasikiliza waganga wa jadi, kufanya uchunguzi wake
binafsi, na kuboresha mchanganyiko wa madawa kwa matibabu. Tunatoa matokeo katika kitabu
kiitwacho “Dawa za asili katika nchi za tropiki.” Kwa hiyo tangu 1985, tumeweka wazi kwa
watu wote ujuzi wetu wote juu ya afya na uponyaji kwa kutumia mimea inayopatikana bure kwa
jamii nzima. Hatuna siri, na hakika hatuna sheria inayozuia kuigwa!
anamed inatoa ujuzi na uzoefu huu, hasa katika Afrika, kwa kuendesha semina za “Dawa za
asili” kwa muda wa juma moja kwa wafanya kazi wa afya, madaktari, waganga wa jadi, viongozi
wa dini, wahudumu wa jamii na kadhalika. Semina inapitia utambuzi na uchunguzi zaidi wa
baadhi ya mimea ya dawa, utayarishaji wa madawa kutokana na mimea hiyo, matumizi yake
katika tiba na matatizo ya kawaida ya kiafya na magonjwa.
Kwa kusema “dawa za asili,” anamed ina maana ya muungano wa faida za madawa ya jadi na
zile za huduma za tiba za kisasa zenye msingi wa kisayansi.
Kitabu kiki, kitabu cha pili katika mfululizo wa “Dawa za asili katika nchi za Tropiki,” ina
karibu masomo yote yanayohitajika kwa mafunzo ya semina kwa juma zima la kwanza katika
dawa za asili. Nafasi hairuhusu maelezo zaidi juu ya falsafa ya kazi yetu, ingawa jambo hili ni la
muhimu sana. Jambo hili limeelezwa katika kitabu cha kwanza, ambacho pia kinaeleza mimea
mengi zaidi na kina maelezo zaidi juu ya kujitengenezea dawa nyumbani. Kitabu cha tatu ni
msaada wenye taarifa nyingi kwa viongozi wa semina. Kitabu cha nne kimetolewa kwa ajili ya
huduma kwa wanaoishi na VVU/UKIMWI.
Sehemu I ya kitabu hiki inaelezea jinsi ya kuzuia baadhi ya matatizo ya kitabibu yaliyo ya
kawaida katika nchi za tropiki, na sehemu ya II ni juu ya kutibu. Sehemu III inaelezea mimea na
miti mitano maalumu, ambayo yote inaweza kustawi katika nchi za tropiki. Kwa miti hii mitano
tu matatizo mengi ya kiafya yanaweza kutibiwa. Kwa nyongeza, unaweza kupata chakula chenye
virutubisho, kusafisha maji, kurutubisha ardhi na kutengeneza kiuatilifu kizuri. Sehemu ya IV
inaeleza jinsi ya kutengeneza baadhi ya madawa. Na sehemu ya V inatoa baadhi ya msaada kwa
ajili ya semina, pamoja na mtiririko muhimu wa rejea kwa ajili ya waganga wa dawa za asili.
Ukishahudhuria semina ya anamed juu ya dawa za asili, tafadhali endelea kuwasiliana na
wengine katika mkoa wako na nchi yako ambao wanatibu kwa madawa ya asili. Panga
kutembeleana, endesha mafundisho, na julisha anamed International huku Ujerumani juu ya
mafanikio yako! Asante!
Sehemu I
Sura 1:
Kuzuia magonjwa ya kawaida.
Kama tukijali mtindo wetu wa maisha, lishe, afya na mazingira tunayoishi tunaweza kutoa
mchango mkubwa sana katika afya bora ya familia zetu, mimea yetu na wanyama.
1.1.Kula vizuri!
Mara nyingi ni tatizo kwamba, watu wakitajirika kidogo, ubora wa lishe yao unashuka.
Vyakula bora (angalia jedwali hapo chini) vinatujengea nguvu na mfumo wetu wa kinga
mwilini – yaani uwezo wetu kushambulia maambukizi na magonjwa. Vyakula visivyo
bora kama vile sukari nyingi, unga uliokobolewa, mkate mweupe, soda mbalimbali,
vyakula vya kwenye makopo, hupelekea ukosefu wa vitamini na protini. Kwa hiyo
tunakuwa na uwezekano mkubwa kupata maambukizi yoyote na magonjwa.
Lima matunda, mbogamboga na mimea ya madawa wewe mwenyewe! Siyo jambo lililopitwa na
wakati wala rahisi! Vyakula vya kujitengenezea kutokana na bustani ya nyumbani ndivyo
vyenye virutubisho bora zaidi.
Lisha watoto mara kadhaa kwa siku. Wanahitaji vyakula kidogo kidogo mara kwa mara.
a) NDOO YA KIJANI: Tupa kila siku: Kwa ajili ya takataka za ki-mimea kutoka bustani
yako au jikoni (“0rganic waste”). Uziozeshe kupata mbolea. Au afadhali zaidi: uwalishe
kuku zako na takataka za ki-mimea ili panya na nyoka wasikaribishwe karibu na nyumba
yako
b) NDOO YA BLUE: Tupa kila wiki: Kwa ajili ya karatasi. Ukusanye kwenye ndoo na mara
moja kwa wiki choma karatasi pamoja na plastiki inayoweza kuchomwa ndani ya dakika 5.
Majivu yatupwe pamoja na metali.
c) NDOO NYEKUNDU: Tupa kila mwezi. Kwa ajili ya metali, vioo, plastiki, betari. Kama
kuna uwezekano wowote wa kuvitumia tena au kuvibadilisha kuwa vitu vingine, fanya
hivyo. Sisitiza serikali yako idai fedha za kuwekesha kwa kila mfuko wa plastiki na chupa za
vioo inayouzwa, ili kwamba ziweze kutumika tena au kurudishwa viwandani. Vikusanye
kwa uangalifu, na kama hakuna mfumo wa kuweza kuvitumia tena kila mwezi uvizike chini
sana kwenye udongo. Betari hasa zina sumu! Usipande mboga zako juu ya shimo hilo!
d) Mbao: Uchome na uweke majivu yake shambani, yana madini yenye thamani.
1.7.Usafi na Afya
Wakati wote osha mikono yako kwa sabuni na maji kabla ya kula au kutayarisha chakula, na baada
ya kutoka chooni. Kama huna sabuni jitengenezee, au sugua mikono yako kwa maji ya majani ya
mpapai.
Kuoga mwili mzima kila jioni hufanya mwili na kitanda kuwa safi.
Tumia kitambaa kilicho safi. Wakati wa dharula, kama unahitaji huduma lakini ukawa huna
kitambaa, chukua vipande vya nguo hasa za pamba. Ili kuzifanya salama zichemshwe katika
maji kwa dakika 20 na zikaushe kwa kutumia kaushio la jua (sola) lililo safi au kama huna
kaushio la jua zikaushe kwa kuanika kwenye kamba ya nguo juani.
A. Vidonda
Lengo kuu la tiba hii ni kuzuia kidonda kupata maambukizi, hivyo kuruhusu mchakato wa mwili
kujiponya wenyewe vizuri iwezekanavyo.
a) Kwanza osha kidonda.
A.2. Vidonda vyenye maambukizo, majipu yaliyopasuka ya siku nyingi, vidonda vya wazi
Papai (Carica Papai)
Kwa matayarisho ya papai yafuatayo, vidonda vya wazi vilivyokuwa sugu kwa miaka mingi
vimeweza kupona, kwa kawaida hata ndani ya wiki 1. Hii ni moja kati ya mifano kadhaa ambapo
dawa za asili zimekuwa bora kuliko madawa ya hospitalini.
Tumia matayarisho yafutayo ya mapapai hadi kidonda kisiwe na usaha tena. Kisha tibu kidonda
kwa sukari au mchanganyiko wa asali na sukari.
A.2.a. Sukari ya papai
Changanya gramu 10 za sukari (nusu ya kikopo cha mikanda ya picha) na matone 10 ya utomvu
wa papai bichi. Tengeneza upya kila siku. Tusemapo sukari „halisi“ tuna maana ya sukari
ambayo imechukuliwa moja kwa moja kutoka kwenye mfuko mpya kwenye kiwanda. Weka hii
sukari ya papai kwa wingi kwenye kidonda, na mara tu inapoanza kuwa na majimaji ongeza
nyingine. Kidonda kinaweza kuhitaji huduma hii mara kadhaa kwa siku.
B. Kuungua
B.1. Kidonda kipya cha kuungua
Kwanza poza kidonda kwa maji safi ya baridi. Kumbuka, lengo kuu la huduma hii ni kuzuia
maambukizo. Mweke mgonjwa kwenye chandarua ili kuzuia inzi kwenye kidonda.
C. Majipu
Jipu ni maambukizo yanayosababisha kifurushi kidogo cha usaha chini ya ngozi.
C.1. Jipu lililofungwa usaha chini ya ngozi, ni pamoja na majipu yaliyo na mdomo,
vidonda vilivyofungwa, maambukizo ya ngozi kuzunguka makucha ya vidole vya mkono
au miguu n.k.
C.1.a. Vitunguu saumu (Allium sativum)
(i) Kata vipande vyembamba vya vitunguu saumu na uvifungie kwenye sehemu iliyoathirika
(fanya hivi kwa usiku mzima kwa siku kadhaa) au
(ii) Pondaponda kitunguu saumu na upake sehemu iliyoathirika au
(iii) Tumia mafuta ya kitunguu saumu (angalia sura 7)
Vitunguu saumu vina nguvu sana kuliko vitunguu maji. Uwe mwangalifu: Mgonjwa mwenye
udhaifu wa ngozi anaweza kupata mabaka. Kufungia kitunguu saumu kwenye ngozi ndiyo njia
bora zaidi, lakini pia iletayo maumivu zaidi. Kupaka ngozi kwa mafuta ya vitunguu saumu ni
tiba dhaifu kidogo lakini pia isiyosababisha maumivu sana.
C.1.b. Dawa ya mafuta ya pilipili: Angalia sura ya 12
Kwa matibabu ya ngozi, tunapendekeza uanze na matibabu rahisi zaidi yanayonawirisha ngozi
(yaliyotajwa mwanzoni), na endelea kwa utaratibu hadi kwenye zile zenye nguvu - lakini pia
madhara - zaidi.
C. Maambukizi ya mba
Maambukizi ya mba yanaweza kutokea kwenye sehemu yoyote ya mwili, lakini mara nyingi
yanapatikana katikati ya vidole vya miguu (athlete’s foot), au vidole vya mikono na katikati ya
paja. Baka (alama nyeupe ya mviringo kichwani) pia ni maambukizi ya mba. Sehemu
zilizoathirika zioshwe kila siku kwa maji na sabuni. Baadaye ziwekwe katika hali ya ukavu na
zihudumiwe kama ilivyoelekezwa hapo chini. Ikiwezekana, ukae kwenye hewa nzuri na mwanga
wa jua. Vaa nguo zilizotengenezwa kutokana na malighafi asilia, yaani pamba. Endelea na
matibabu hayo mpaka majuma 2 baada ya dalili kupotea.
C.1. Vigunguu saumu (Allium sativum)
Sugua mafuta ya vitunguu saumu (angalia sura ya 7.5) kwenye sehemu iliyoathirika. Kwa mba
wa kwenye vidole vya miguu unaweza kuweka kikonyo cha kitunguu saumu katikati ya vidole
vya miguu.
C.2. Ringworm bush (Cassia alata) na mbono au mafuta ya mawese.
Twanga majani mabichi ya Cassia alata, na uchanganye vijiko vyake 10 na kijiko 1 cha mafuta
ya mbono. Kama mafuta ya mbono hayapatikani, tumia mafuta ya mawese au mafuta mengine
ya mimea. Weka mara 3 kila siku. Tengeneza upya kila siku. Kama huna mafuta kabisa, twanga
haya majani mabichi na uyasugue kwenye sehemu iliyoathirika mara 3 kwa siku.
C.3. Ringworm bush (Cassia alata), papai na mafuta
Twanga kiganja kizima cha majani mabichi na machanga ya ringworm bush, ongeza matone 10
ya utomvu wa papai bichi na kijiko kizima cha mezani cha mafuta ya mbono au ya mawese.
Changanya na usugue kwenye sehemu iliyoathirika mara 3 kwa siku. Tengeneza dawa mpya kila
siku.
C.4. Dawa ya mafuta ya kuzuia mba. Tumia mwarobaini, melia au ringwormbush (Angalia
sura ya 12).
D. Upele (Scabies)
Upele hutambulishwa na uvimbe mdogomdogo unaowasha, ambao unaweza kutokea mwili mzima.
Katikati ya uvimbe huu kuna vipele vyeusi vidogovidogo zaidi vyenye vichwa vyenye ukubwa wa
vichwa vya sindano. Upele ni kawaida kwa watoto. Unapatikana zaidi katikati ya vidole vya
mikono, kwenye kiungo cha mkono na kitanga, kiuno, na sehemu za siri. Husababishwa na vijidudu
vidogo vinavyotengeneza njia chini ya ngozi. Unaambukiza kwa urahisi sana. Kama mtu mmoja
katika familia akiwa na upele, lazima familia nzima itibiwe. Usafi ni muhimu. Oga mwili mzima na
badilisha nguo zako kila siku. Nguo zote na matandiko lazima yafuliwe na kuanikwa juani. Njia
rahisi ni kuziweka kwenye jiko la jua. Safisha sehemu za chuma au za mbao za kitanda chako kwa
mafuta ya taa.
SURA 4: KUHARISHA
Mtu anaharisha wakati haja kubwa inapokuwa ya majimaji. Kama haja kubwa pia itakuwa na
kamasi na damu, tatizo linaitwa “kuharisha damu” (Dysentry).
Kuharisha ni ugonjwa hatari sana. Inahusika na vifo vya zaidi ya watoto millioni 3 katika nchi
zinazoendelea kwa mwaka. Karibu mara zote watoto wasingekufa – kama tu wazazi wao au hata
klinki zingejua matibabu yaliyoelezwa katika sura hii. Kuharisha ni hatari hasa kwa watoto
waliopungukiwa lishe.
Kuharisha kunaweza kuwa dalili za magonjwa mengine, ambayo pia yanahitaji matibabu,
angalia jedwali hapo chini 4.1. Kama ukienda chooni mara moja, lakini ukakaa huko siku nzima,
una kipindupindu!
Watoto wanapoharisha, wakati wote wapewe maji ya chumvi (Oral)! Watu wazima wangependa
kwanza kujaribu dawa rahisi zaidi kama vile dawa ya mkaa, matunda ya mpera mabichi n.k.,
lakini kama kuharisha kukiendelea, au kwa matatizo makubwa zaidi, maji ya chumvi ni ya
lazima kwa watu wazima pia! Mgonjwa lazima aendelee kula vyakula vinavyoongeza vitamini
na madini ya kutosha.
Mara nyingi kuharisha kunaweza kuzuiwa, hasa kwa kujali suala la usafi.
MAJI: Tumia maji mazuri, kama hakuna maji safi ya chemchemi, tumia maji
yaliyochemshwa au tengeneza chai ya majani ya mpera na uitumie badala ya maji.
SUKARI: Hasa tumia asali, isipokuwa kwa watoto walio chini ya mwaka mmoja, ambao
kwao haishauriwi kutumia asali. Kama hakuna asali, tumia sukari ya nyumbani (baadhi
ya hospitali zinatumia glucose). Kama huna sukari au mgonjwa ana kisukari, badala ya
gramu 30 za sukari kwenye mchanganyiko ulioelezwa hapo chini (A 2), unaweza
kutumia na kuchanganya vizuri moja kati ya vifuatavyo katika lita 1 ya maji:
a) Gramu 100 za ndizi tamu zilizosagwa (kama nusu kiganja, usichemshe).
b) Gramu 100 za viazi vitamu (kama nusu kiganja, chemsha kwa dakika 10).
c) Gramu 30 (vijiko 3 vya chai vilivyojaa sana) vya unga wa ngano, mchele
uliotwangwa au mtama. Chemsha kwa dakika 5.
CHUMVI: Hasa, tumia ile inayoitwa “chumvi ya kienyeji.” Hii inatengenezwa kwa
kienyeji kwa kuchukua majivu ya miti iliyochomwa, ongeza maji, chemsha hadi maji
yakauke kwenye chungu cha udongo (kwa sababu vyombo vya metali vinaweza
kuharibika) na kukusanya chembechembe zinazojitokeza. Hii ni nzuri, kwa sababu ina
potassium. Ama sivyo tumia chumvi ya mezani (sodium chloride).
POTASSIUM: Ni kitu kinachopaswa kuongezwa kama chumvi ya mezani ikitumika na
kama kuharisha kutaendelea kwa siku kadhaa. Potassium inasaidia misuli ya utumbo na
matumbo kufanya kazi vizuri. Vyanzo vizuri vya potassium ni pamoja na mchicha, embe-
mafuta, ndizi, boga, maji ya nazi, karoti, soya iliyopikwa, njugu, moringa na majani ya
mboga za kijani-nyeusi yaliyochemshwa.
Kwa watoto wadogo ambao hawawezi kula chakula kingi, ongeza kijiko 1 cha chai cha
majivu safi (kutokana na miti au nyasi zisizo na sumu, au kutokana na magugu maji
yaliyokaushwa, ambayo yana potassium nyingi) kwenye lita 1 ya maji inayotumika
kutengenezea maji-chumvi (angalia chini). Baada ya dakika kadhaa, chuja maji.
Kama chochote kati ya vifaa vyako (maji, sukari au chumvi) siyo safi kikamilifu,
chemsha mchanganyiko huo kwa dakika chache ili kuua bacteria. Nyongeza ya rangi na
harufu havisaidii kwa lolote.
Chemsha kwa dakika 2 katika lita 1 ya maji, na uache ikolee kwa dakika nyingine 30.
Kama mwembe au mpera haupatikani tumia majani ya mpapai. Lakini chai hiyo itakuwa
chungu na mtoto anaweza kuikataa.
Kunywa kiasi hiki cha chai kwa masaa 24. Endelea kwa siku 8 hata kama dalili
zimetoweka. Tiba inayoendelezwa huondoa mayai yaani amiba kutoka kwenye matumbo.
Mara nyingi inaondoa minyoo ya kwenye matumbo pia.
Bakavu, huko Kongo, mahali ambako kumbukumbu zimetunzwa kwa uangalifu, walikuwa
na mafaniko ya 99% katika kutibu zaidi ya wagonjwa 200 wanaosumbuliwa na amiba na
kuharisha damu kwa kutumia chai ya majani ya Euphorbia Hirta, mpera na mwembe.
Dokezo kwa Mahospitali: Unaweza kupendelea kutayarisha chai hii ya kuharisha ya anamed
kutokana na majani makavu. Vuna mimea hii kwa kiwango kilicho sawa kuelekea mwisho wa kipindi
cha mvua, ikaushe vizuri na uisage. Kipimo sasa kitakuwa kuchemsha kijiko 1 kilichojaa katika lita 1
ya maji kwa dakika 2 na baadaye uache ikolee kwa dakika nyingine 30. Kama unga wa majani makavu
ukitunzwa kwenye chombo kisichoruhusu hewa kuingia, itadumu salama kwa mwaka mmoja .
SURA 5: MALARIA
5.1. Utangulizi
Katika dunia nzima karibu watu milioni 500 hupata malaria kila mwaka. Kati ya hao, millioni 1
hadi 2 hufa. Wengi kati yao ni watoto chini ya miaka 5.
Malaria huambukizwa kutoka mtu mmoja hadi mwingine na mbu wa jamii ya Anopheles.
Wanapochukua damu kutoka kwa mtu aliyeambukizwa wanachukua vimelea vya malaria
(vijidudu viitwavyo plasmodium). Kisha wanapochukua damu kutoka kwa mtu mwingine,
wanaingiza plasmodium pamoja na mate yao. Plasmodium husafiri hadi kwenye ini, na kutokea
hapo huingia hadi kwenye chembe nyekundu za damu. Mtu huugua baada ya siku 7 hadi 10
baada ya kuumwa na mbu.
Kwa kawaida mgonjwa wa malaria huhisi baridi na mara nyingine hutoka jasho. Inawezekana
lakini kwamba dalili mojawapo ikawa na nguvu zaidi, kiasi kwamba haidhihiriki haraka kwamba
mgonjwa ana malaria. Kwa njia hii malaria inaweza kujificha nyuma ya safu ya dalili za
magonjwa, mfano: kuharisha na kutapika, matatizo ya kiakili, kupoteza fahamu, upungufu wa
damu au homa.
Mimea inayotibu inaweza kuokoa maisha ya wengi. Mfano wa kushangaza unatokea Kongo
D.R.C.: Mwaka 1997 Askofu wa Dayosisi ya Bolungu–Ikela ilimbidi kuwakimbia waasi na
kujificha porini kwa majuma 4, akiwa na watu wengine 20. Hawakuwa na nyumba wala
chandarua, wala madawa. Waliishi chini ya miti! Walipopata homa walikunywa chai za dawa
zilizoorodheswa hapa chini. Askofu alisema, “Pamoja na hofu yetu, hakuna mmoja wetu
aliyekuwa mgonjwa sana kwa malaria.”
Muhtasari wa matibabu
1. Watu wazima wanatakiwa kunywa jumla ya lita 3 kwa siku. Watoto nao ni lazima pia
wanywe sana kiwango kikitegemea uzito wa miili yao.
2. Chai ya dawa inaweza kutengenezwa kwa kuchemsha dawa katika maji au kumwagia maji
ya moto.
Kumwagia maji ya moto (Infusion): Mwaga lita 1 ya maji yanayochemka kwa kiganja
kizima cha majani mabichi ya dawa, au gramu 15 ya majani makavu (kama ni Artemisa
annua au Azadirachta indica iwe gramu 5). Iache kwa dakika 10 hivi, kisha ichuje.
Kuchemsha (Decoction): Kipimo ni kama katika kumwagia maji ya moto. Chemsha
maji na mimea kwa pamoja kwa dakika kama 20 hivi. Poza na uchuje.
3. Kwa mchaichai, chemsha majani yake kwa dakika 2. Acha itulie kwa angalau dakika 10,
kisha ichuje.
4. Vernonia amygdalina. Majani yake ni machungu sana. Magamba ya mizizi yake lina nguvu
zaidi. Tumia mizizi yenye unene wa kidole, mizizi ya pembeni, siyo mzizi mkuu, ili mti
usife. Tumia kiganja 1 cha magamba ya mizizi na uchemshe kwenye lita 1 ya maji kwa
dakika 20. Chuja na unywe kwa awamu 4 kwa siku 1. Endeleza tiba hii kwa siku 7.
5. Cinchona officinalis: Chemsha gram 10 au vijiko 3 vya chai vya magamba
yaliyopondwapondwa katika lita 1 ya maji kwa dakika 10, chuja na unywe kwa awamu ndani
ya masaa 24. Watoto wanywe kiasi kidogo zaidi kufuatana na uzito wao.
6. Katika hali ambayo mimea yote hii haisaidii, endelea kutumia lita 2 za mchaichai kila siku,
na pia tumia dawa za hospitalini (k.mf. Amodiaquine au Fansidar). Hakikisha pia kwamba ni
malaria kweli inayomsumbua mgonjwa na si ugonjwa mwingine.
7. Kumbuka kuwa hakuna wagonjwa wawili wanaoweza kuwa na hali zilizo sawasawa kamwe.
Ingawa watu wawili wanaweza kuwa na dalili zile zile, wanaweza wasitibiwe na dawa ile ile
ya mmea.
8. Akina mama wajawazito wasitumie Azadirachta indica (mwarobaini) au Vernonia
amygdalina (mtukutu). Katika miezi 3 ya mwanzo ya ujauzito tumia Cinchona officinalis
(mkwinini) au Artemisia annua chini ya uangalizi wa Daktari tu.
Ili kudumu katika afya njema, kila mtu anatakiwa kuhakikisha mfumo wake wa kinga mwilini
uko imara kadri iwezekanavyo. Jambo hili ni la muhimu hasa kwa watoto wadogo, wajawazito
na watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (VVU).
Mimea na mazao ya asili yafuatayo yanasaidia kuimarisha mfumo wa kinga mwilini. Vinafaa
kwetu sote. Kama unaishi na VVU, tumia mimea miwili au mitatu kati ya ifuatayo. Washiriki
wa anamed katika nchi nyingi wametoa taarifa za mafanikio mazuri katika matumizi ya kila siku
ya unga wa majani ya mlonge na chai ya artemisia – bila kujali kama wanatumia madawa ya
kupunguza makali ya VVU (ARV´s) au la.
3. Artemisia annua
Washiriki wa anamed wanaoishi na VVU walitumia chai ya artemisia kama ifuatavyo:
a) Wakati wa hali mbaya ya ayfa (acute phase): Mwaga maji ya moto kwenye gramu 5 (yaani
vijiko 4 vya chai vilivyojaa sana) za majani makavu ya artemisia, acha itulie kwa dakika 15,
chuja na unywe chai hii kwa awamu 4 ndani ya siku moja. Kutegemea hali ya mgonjwa njia hii
inaweza kuendelea kwa muda wa wiki kadhaa au hata miezi.
b) Baada ya hapo (chronic phase): Mwaga robo lita ya maji ya moto kwenye gramu 1,25 (yaani
kijiko 1 cha chai) ya majani makavu ya Artemisia, acha itulie kwa angalau dakika 15, chuja na
unywe chai hii wakati wa asubuhi. Unaweza kuendelea hivyo kwa wiki au hata miaka.
Kama una mimea ya Artemisia kwenye bustani yako unaweza kutumia gramu 25 (acute phase)
au gramu 6,25 (chronic phase) ya majani mabichi kila siku.
Propolis: Gundi hii ni fukizo la kiasili linalotengenezwa na nyuki katika mizinga yao, na
imeonekana kuwa ni antibiotic, anti-fungal, antiseptic na antiviral. Changanya gramu 10 za
propolis na ml 100 za kileo halisi cha kutengenezea dawa (98%) kwa matumizi ya ndani
(kunywa). Tikisa mara moja kwa siku kwa muda wa siku 30. Chuja. Kipimo: kunywa matone 20
mara 1 hadi mara 3 kwa siku.
Kwa maelezo zaidi angalia katika kitabu cha anamed “Ukimwi na madawa ya asili”
SEHEMU III: MATUMIZI YA BAADHI YA MIMEA MUHIMU
KATIKA ENEO LA TROPIKI
7.2. Ulimaji
Vitunguu saumu hupendelea udongo wenye rutuba unaopitisha maji vizuri. Pogoa kikonyo kwa
uangalifu kutoka kwenye shina la saumu, na ukipande kwenye eneo yenye kivuli kwa kina cha
sm 5, na umbali wa sm 15 mche hadi mche kwenye mstari wa sm 30 mstari hadi mstari. Kama
mmea ukianza kutoa maua likate ua kusudi nguvu ya mmea iende kustawisha shina. Vuna wakati
majani yakianza kuwa na rangi ya hudhurungi na kuanza kunyauka. Kausha vitunguu kivulini
mahali ambapo kuna hewa nzuri inayopita, na kwa uangalifu vifute udongo na majani ya juu
(ukifanya hivi wakati vitunguu vina unyevu, vikonyo vitaharibika). Vitunze katika chombo cha
udongo.
7.4. Vilivyomo:
Allicin: Vitunguu saumu vinaposagwa, enzaimu alliinase inaibadilisha alliin na kuwa allicin.
Allicin ni dawa ya bakteria na fangasi yenye nguvu. Alisini pia inatibu kukaza kwa mishipa ya
moyo (Arteriosclerosis).
Ajoene: Pamoja na kuwa na asili ya kuua vidudu na fangasi (anti-bacterial na antifungal) pia
inazuia kuganda kwa damu na kupunguza uwezekano wa kutokea magonjwa ya moyo
Flavonoids: Ni vizuizi vya kupotea kwa oksijeni na inapunguza hatari za saratani, magonjwa ya
moyo na baadhi ya magonjwa ya mishipa ya fahamu.
Wakati wa maambukizo ya watu wengi ya ugonjwa wa uti wa mgongo katika eneo fulani huko
Ethiopia, wenyeji wa eneo hilo walihamasishwa kula vitunguu saumu vibichi. Kati ya wale
waliokula hakuna aliyekufa, lakini wale wengine wengi wao walikufa. Harufu ya vitunguu
saumu katika pumzi ya mtu inaweza kupunguzwa kwa kula tangawizi kwa njia yoyote.
8.2. Ulimaji
Hifadhi mbegu zikiwa kavu na zidumu kuwa kavu.
Tumia kiasi chake kidogo sasa, na kilichobaki kwa kila mwezi. Kama zikitunzwa katika hali ya
ukavu kabisa, hazitaharibika. Kiwango cha kuota kinapungua kwa 10% kwa mwaka. Mbegu na
miche inayozaliwa ni midogo sana na dhaifu. Vinahitaji uangalizi mkubwa! Usijaribu kulima A
– 3 mpaka wewe au mtunza bustani yako awe amejitayarisha kutoa muda wake mwingi kwa
jambo hili, ni pamoja na Jumamosi na Jumapili.
Weka tabaka la udongo mzuri lenye unene wa sm 3 kwenye kitako cha trei, na ufunike kwa
tabaka nyingine la mchanga la sm 3. Mchanga huu uchemshwe kwa dakika lisizopungua 5 ili
kuua mbegu za magugu ambazo zinaweza kuwemo. Mbegu zenyewe zina virutubisho vya
kutosha vinavyohitajika wakati wa hatua za mwanzo za kukua.
Hakikisha kwamba kitalu kina unyevu sana lakini hakina maji yaliyotua. Mbegu zisambazwe
kwa usawa kwenye uso wa udongo – chujio la jikoni linaweza kusaidia mchakato huu. Usifunike
mbegu.
Kuhamishia shambani
Mimea ikifikia urefu wa sm 15, kama majuma 8 baada ya kupanda, tayarisha
shamba lako.
Artemisia hustawi vizuri katika aina mbalimbali za udongo na hali ya hewa.
Inastawi vizuri zaidi katika udongo wa hali ya kati au wa hali ya “alkaline” kidogo,
lakini inavumilia udongo wenye hali ya acid kidogo.
Zao zuri kulima kabla ya artemisia ni viazi vitamu au viazi mviringo, kwa sababu
viazi huufanya udongo uingize hewa nzuri . Artemisia ni mmea wa jalalani, maana
yake ni kwamba inastawi vizuri kwenye udongo unaopitisha hewa vizuri ambao una
nitrojeni nyingi kama vile udongo kutoka kwenye rundo la mboji. Kwa hiyo lainisha udongo.
Kama ardhi ni ngumu sana na ina udongo wa mfinyanzi, chimba kwanza shimo ambalo ni kubwa
zaidi sana ya kipimo ulichotaka, tuseme sm 70 × sm 70 × sm 70 na ndani yake tupia vijiti na
majani mengi (lakini siyo yatakayo katika mimea yenye “acid” kama vile conifers au mkaratusi)
na kwenye udongo changanya mbolea iliyooza ambayo ina kinyesi cha ng’ombe au kuku. Kama
ukipanda miche ya artemisia kwa umbali wa sm 60 toka mche hadi mche, utapata miche 30,000
katika hekta. Kama nafasi itaruhusu panda kwa umbali wa meta 1. Kati ya miche ya artemisia
unaweza kupanda maharage au karanga, ambavyo hurutubisha udongo, au panda mpapai,
mahindi au mtama katika mistari kwa kubadilishana na mstari wa artemisia. Katika udongo
wenye rutuba artemisia itakua na kufikia upande wa meta 1 na urefu wa meta 3!
Badala ya kupanda artemisia katika shamba moja kubwa, ipande katika maeneo mbalimbali,
kwenye jua, kwenye kivuli, karibu na mlima, kwenye ardhi tambarare, ili ugundue mwenyewe ni
sehemu ipi inayofaa zaidi. Kwenye eneo lenye joto ni bora zaidi ardhi ikikaa na unyevu. Kama
joto litakuwa zaidi ya nyuzi 30º wakati wote na hakuna uwezekano wa kumwagilia wakati wote,
tengeneza kivuli. Hili linawezekana kwa kutengeneza kiunzi cha mianzi ambacho kwacho
unaweza kustawisha mimea yenye virutubisho kama maharage yanayotambaa, Passion fruit na
maboga, au kwa kubadilishana katika mistari kati ya mistari ya A – 3, na mistari ya mapapai au
mahindi.
Kama unaishi katika eneo kame sana, pandikiza miche kwenye mistari kama sm 5 chini ya uso
wa ardhi. Kama unaishi katika eneo ambalo mara nyingine maji hutua kwa siku kadhaa
mfululizo, panda miche kwenye mistari juu kidogo ya usawa wa kawaida wa ardhi.
Tumia jembe na umwagilie mara kwa mara. Ardhi lazima ikae na unyevu, hasa majuma 2 ya
kwanza baada ya kupanda. Mmea huitikia matatizo, hasa ya ukame mkali, kwa kutoa maua kabla
ya kukomaa. Mimea ikifikia sm 50 kwa urefu, unaweza kuiwekea mbolea ya asili, kama vile
kinyesi cha wanyama kilichoozeshwa vizuri. Tumia mbolea za viwandani pale tu unapokuwa
huna njia nyingine. Kwa hali hii, jaribu kutumia mbolea ya N-P-K.
Njia mbadala (stone-method), wakati mmea ukifikia urefu wa sm 50, ni kupinda matawi ya chini
na kuzika sehemu zake za kati kwa udongo. Jiwe linaweza kuhitajika kuzuia lisifyatuke. Mara tu
tawi lililozikwa likianza kuota mizizi, likate kutoka kwenye shina mama na ulipande shambani.
Kama kawaida tumia mmea wenye afya zaidi, na mimea isiyo na maua pekee au hata vitumba.
1. Changanya vikombe kumi kumi kila kimoja cha udongo, mchanga na maji.
2. Chemsha mchanganyiko huu kuua mbegu za magugu.
3. Tengenza kitalu kinachochukulika kutokana na miti na uweke vitundu vidogovidogo kwenye kitako.
4. Weka udongo kwenye kitalu.
5. Fungua mfuko wenye mbegu – ambazo ni ndogo sana!!
6. Sambaza mbegu kwa usawa. Usizifunike, na uweke kitalu kwenye sehemu yenye mwanga. Udongo
ukianza kukauka, weka kitalu ndani ya maji.
7. Mbegu huota kati ya siku 3 hadi 7. Zinahitaji jua la kutosha.
8. Punguza mimea.
Mara nyingine mchwa huunda kiota chao kuzunguka shina la artemisia. Kama hali hii ikizidi
sana kuwa tatizo, jaza ndoo kwa majani na mashina ya mimea yenye protini, mfano: kibaazi,
tithonia, au lesena, acha vitulie kwa juma 1 na uvimwage kuzunguka shina.
Mpango unaowezekana kwa nchi za kusini.
Wakati wowote wa mwaka, siha sehemu kidogo ya mbegu halisi kutoka anamed. Kama unakaa
sehemu za milimani, lima artemisia mwaka mzima. Kama unaishi kwenye nchi zenye joto, za
bondeni, lima artemisia kivulini. Mfano: Panda katika mistari kwa kubadilisha, mstari wa
artemisia ukifuatiwa na mstari wa mahindi, kisha wa artemisia tena. Au vizuri zaidi: Siha
artemisia wakati wa mvua, ipandikize mwanzo wa kipindi cha ukame na uimwagilie!
8.3. Uvunaji
Vuna majani yote wakati vifundo vya maua vinapoanza. Artemisimin ni nyingi zaidi kabla
kidogo maua haujachania. Mabaki ya mavuno yake yanaweza kufanywa mboji au kulishwa
wanyama.
Jinsi ya kufanya:
Kwa mkono mmoja, shikilia kwa nguvu mwisho wa tawi, kwa mkono mwingine, purura majani
kutoka kwa ncha hadi kitakoni. Unaweza kupenda kuvaa kifuko cha mkono. Ondoa matawi yote
kwenye mavuno yako. Unaweza kutumia majani haya mabichi hapohapo kutibu malaria. Ama,
laza majani kwenye ubao, na kwa kisu kikali, yakatekate vipande vidogo vidogo vyenye urefu
wa sm 1 (kama jinsi Afrika tunavyokatakata mboga za majani). Yakaushe kwa makini
iwezekanavyo katika siku 3 kwa joto lisilozidi nyuzi 40ºC. Kama hewa ina unyevu, yakaushie
kwenye jua, kama ni kavu basi kaushia kivulini. Kwa vyovyote majani lazima yakaushwe ndani
ya siku 3. Wakati yanakauka ondoa vijiti vilivyosalia kwa kusugua majani kwenye chekecheo
lenye nafasi kama za waya wa kuzuia mbu madirishani. Unaweza kujitengenezea chekecheo
nyumbani kwa kutumia waya huo.
Kausha unyevu hadi kipima unyevu, kilichowekwa katika mfuko wa plastiki pamoja na majani,
kitakapoonyesha kiwango cha unyevu kisichozidi 40 % katika nchi za kusini.
Ni vigumu kukadiria mavuno ya zao jipya lililolimwa kwenye eneo jipya. Katika hali nzuri
kabisa ya hewa kwa uzalishaji, kila mmea unatoa gramu 400 za majani makavu. Kwa jinsi hiyo
mmea mmoja unaweza kutumika kutibu karibu wagonjwa 11 (gramu 35 kila mmoja).
Kuhifadhi: Hifadhi kwenye giza, kwenye chombo kisichopitisha hewa kama vile plastiki au
pipa la metali. Weka kipima unyevu katika chombo hicho. Kama kipima unyevu kikionyesha
unyevu kuwa 40%, basi majani yana maji 4% na yatadumu kwa mwaka 1. Kama ni 30%, majani
yana maji 3% na yatadumu miaka 3.
Ubora: Majani yanatengeneza chai yenye ubora kama hayana vitawi au maua, rangi ni kijani
iliyokolea sana (nyeusi) na siyo ya kijivu au hudhurungi, na yaliyokaushwa vizuri.
Upakiaji: Pakia katika vifuko vya gramu 50 visivyopitisha hewa. Kwenye label juu ya kifuko
andika tarehe ya mwisho kutumika ambayo kwa majani yaliyokaushwa vizuri na vifuko
visivyopitisha hewa (vinavyozuia unyevu pia) iwe mwaka 1 kufuatia wakati wa upakiaji.
Taarifu serikali ! Kama artemisia haijaanza kulimwa katika nchi yako, jaribu kupata kibali
maalumu cha kuistawisha. Itaarifu Wizara ya Kilimo kwamba artemisia tayari inalimwa na
washiriki wa anamed katika nchi zaidi ya 70. Kama ni muhimu mwombe Askofu wako
akuombee kibali Wizarani.
Tembelea wawakilishi wa Shirika la Afya duniani (WHO) na Wizara ya Afya katika nchi yako,
waonyeshe cheti chetu na mimea yako. Hakika utasifiwa!
Neno la faraja – na tahadhari: anamed inaweza kuokoa maisha ya watu wengi zaidi kwa
artemisia kuliko kwa mmea mwingine wowote! Chai iliyotengenezwa kwa majani ya artemisia
annua imekuwa ikitumika China kutibu homa kwa zaidi ya miaka 2000. January 2006, shirika la
Swiss Pharmaceutical Company “Novartis” lilitangaza kwamba lililenga kuzalisha dozi milioni
100 za dawa ya malaria aina ya Coartem (artemether/lumefantrine) mwaka 2006 (kutoka milioni
30 za 2005). Wanadai kwamba dawa hii inatibu kwa 95%. Pamoja na hayo, ni vizuri kusisitiza
kwamba kila dawa - iwe ya kikemia au ya kibailojia - ina kipimo cha mafanikio. Itakuwa ni
makosa kwa mtu kuweka imani yote kwa aina moja tu ya dawa, iwe ya vidonge au ya mimea.
Mafanikio maalumu ya anamed yalikuwa ni kuhakikisha kwamba chai iliyotengenezwa kwa
mmea chotara maalum A-3 inafaa sana katika tiba ya malaria. Chai ya Artemisia yenyewe ni
dawa mchanganyiko, kwa sababu ina dawa 10 tofautitofauti zinazohusika na kutibu malaria.
Dozi tunazotumia zimetokana na zile zilizotajwa katika “IX Chinese book of drugs,” taarifa
zilizo katika kitabu cha Hagers na katika uchunguzi wetu kwenye Chuo Kikuu cha Tuebingen
huko Ujerumani. Tunaweza kudondoa kumbukumbu za Zahanati 3 huko Congo. Waafrika 161
walijitolea kutibiwa kwa kutumia chai ya artemisia. Baada ya siku 5 – 7, 91% kati yao
hawakuwa na vidudu vya malaria kabisa.
Tahadhari: Usitengeneze chai ya artemisia kwenye chombo cha chuma, kwa kuwa
artemisinin huingiliana na chuma!
Hata hivyo ni vizuri kujitengenezea mizani yako: Ning’iniza vikombe 2 vya plastiki
kushoto na kulia mwa kipande cha mti kama ilivyoelezwa katika kitabu chetu
kiitwacho “Madawa ya asili katika nchi za joto: Vikorokoro vya walimu IV, toleo
namba 113”. Kwenye kikombe cha kushoto, weka karatasi 5 za kawaida A 4 (zenye
uzito wa gramu 80 kwa meta za mraba, yaani gramu 5 kwa hizo karatasi). Kwenye
kikombe cha mkono wa kulia weka majani mabichi ya artemisia. Kama mizani
italingana, utakuwa na gramu 25 za artemisia!
H. Matayarisho ya “Chai ya artemisia ya anamed.”
Mwaga lita 1 ya maji yanayochemka kwenye gramu 5 za majani makavu au gramu 25
za majani mabichi ya artemisia. Acha itulie kwa dakika zisizopungua 15, kisha chuja.
Tayarisha chai mpya kila siku. Lazima chai itumike ndani ya masaa 24 tu.
I. Kama hupendi ule uchungu wa artemisia: Ponda majani mabichi. Kila asubuhi na
jioni changanya gramu 2,5 ya unga wake kwenye yoghurt, peanut butter au ndizi
zilizopondwa na ule unga ndani yake. Kunywa maji baadaye.
J. Sukari katika chai: Kwa kawaida tunapinga uwekaji wa sukari katika chai kwa sababu
inasababisha kuoza meno. Kwa upande wa malaria, walakini vijidudu vya malaria
huharibu sukari iliyo katika damu, kwa hiyo kwa watoto walio na umri hadi mwaka 1,
unaweza kuongeza sukari kwenye chai ya artemisia. Kwa watoto wakubwa weka
asali au sukari. Lakini weka sukari au asali pale chai hii itakapokunywewa, ama
sivyo, kwa siku hiyo, vidudu vinaweza kuzaliana katika chai.
K. Asali: Kwa kawaida tunapendekeza kuchanganya chai zetu na asali badala ya sukari.
Haishauriwi kuwapa asali watoto walio chini ya miezi 12. Kwa watoto walio zaidi ya
mwaka 1 ni vizuri sana kuchanganya majani makavu ya artemisia moja kwa moja na
asali na kumpa mgonjwa. Walakini mchanganyiko huu unatakiwa kutengenezwa
upya kila siku.
L. Kutayarisha “sukari ya artemisia ya anamed.”:
Kwa kuwa mchanganyiko utatumiwa na watoto, unatakiwa uwe na mchanganyiko
ulio safi kabisa.
Osha mikono kabla ya kuvuna, na uchukue majani kutoka kwenye sehemu ya juu ya
mmea iliyo safi zaidi. Osha majani kwa uangalifu, yakate na kuyakausha kwenye
meza safi. Yasage hadi yawe laini kabisa kwa kutumia vifaa safi. (Unaweza kutumia
kifaa cha umeme cha kusagia kama kinapatikana).
Chemsha sukari kwenye kikaangio ili kuwa na uhakika kwamba vijidudu vyote
vimekufa na sukari imekauka. Mara tu sukari inapokauka, changanya gramu 10 za
unga wa artemisia kwa gramu 90 za sukari. Kama huna mizani, hii ni sawa na
kuchanganya kikomo cha mkanda wa picha za kamera cha unga wa artemisia ulio
laini sana na vikopo 3 vya namna hiyo vya sukari. Kijiko cha chai kilichosawazishwa
cha mchanganyiko huu kina uzito wa gramu 3 na ni sawa na gramu 0.3 za artemisia
kavu.
Mwisho wa kutumika: Baada ya mwaka 1 kama imetunzwa katika chombo
kisichopitisha hewa.
M. Kuinika: Msimamie mgonjwa ili kuhakikisha kwamba dawa uliyomwinika haitoki.
Kama ikitokwa kwa kupitia njia hiyo hiyo ya haja kubwa katika dakika 30 za kwanza,
mwekee kiasi kile kile cha dawa tena.
MATIBABU
1. Mjamzito katika miezi mitatu ya kwanza
Chini ya uangalizi wa Daktari unaruhusiwa kutumia chai ya artemisia ya anamed. Au unaweza
kutumia vidonge vya quinine (mg 10 kwa kila kilo ya uzito wako, mara 3 kwa siku, kwa siku 7).
Pia kunywa lita 2 za chai ya mchaichai kila siku.
2. Mjamzito katika mwezi wa 4 – 6 au 7 – 9.
Kama kuna daktari, mwombe ushauri wake. Unaweza kutumia chai ya artemia ya anamed,”
(angalia maelezo H hapo juu). Kunywa lita 1 kila siku kwa angalau siku 7. Pia kunywa lita 2 za
chai ya mchaichai kila siku. Ikibidi unaweza kuongeza vidonge vya quinine (mg 10 za quinine
kwa kila kilo ya uzito mara 3 kwa siku, kwa siku 7).
3. Kina mama wanyonyeshao
Unaweza kutumia “Chai ya artemisia ya anamed”, (Angalia maelezo H hapo juu). Kunywa lita 1
kila siku kwa siku zisizopungua 7. Pia kunywa lita 2 za chai ya mchaichai kila siku. Ikibidi
unaweza kuongeza vidonge vya quinine (mg 10 kwa kila kilo ya uzito mara 3 kwa siki, kwa siku
7, au vidonge 3 vya SP (sulfadoxin-pyrimethamine – jina la ki-biashara: Fansidar ).
Kama mgonjwa hawezi kunywa, jaribu njia hii: Mwaga ml 500 za maji kwenye gramu 10 za
majani makavu au katika gramu 50 za majani mabichi, subiri angalau dakika 15, chuja na utumie
njia ya kuinuka (enema) (kwa kuigawa dawa sehemu 4 au zaidi). Ikibidi, unaweza kuchanganya
kwa kuyeyusha vidonge vya quinine, au quinine ya maji katika artemisia hii ya kuinikia.
Yeyusha mg. 30 za quinine kwa kila kilo ya uzito wa mtu katika ml 500 za dawa ya maji ya
kuinikia. Tumia dawa hii ya kuinikia kwa siku 7, au hadi hapo mgonjwa atakapoweza kunywa
tena, yaani wakati ambapo dawa itanywewa kama chai.
Kama mtoto amepoteza fahamu, jaribu njia ifuatayo: Chukua quinine ya maji, au yeyusha katika
ml 50 za maji mg 30 za quinine vidonge kwa kila kilo ya uzito wa mtoto kwa siku, gawanya
katika sehemu 4 au zaidi na umwinike mgonjwa kwa siku hiyo moja. Acha kumwinika mara tu
mgonjwa apatapo fahamu, kisha mpe dawa inayotakiwa kwa njia ya mdomo.
Kama hakuna quinine, unaweza kujaribu kumwinika kwa kutumia artemisia. Changanya ml 50
za maji yanayochemka katika gramu 1 ya majani makavu au gram 5 za majani mabichi, subiri
dakika 15, chuja, na uache ipoe. Tumia chai hii kwa kuinika, ikiwa imegawanywa katika sehemu
4 au zaidi za dozi katika siku 1. Rudia njia hii kwa siku 7, au hadi wakati mgonjwa atakapoweza
kunywa tena. Wakati huo, nunua dawa nyingine kwa sababu artemisia pekee yawezekana
isitoshe kwa mtoto huyu.
Toa nusu ya kidonge cha sulfa – pyri mara moja, au kiasi cha chloroquine mg 250
iliyogawanywa katika siku tatu, au dozi ya amodiaquine mg 250 iliyogawanywa katika siku 3 au
kidonge 1 cha ALU mara 2 kwa siku kwa siku 3. Mpe mtoto vinywaji vingi (maji
yaliyochemshwa, maziwa ya mama). Kama dawa hizi hazipatikani au hazifanyi kazi mwilini,
tumia artemisia. Kama mtoto anakubali kunywa chai hii, mpe ml. 50 za “chai ya artemisia ya
anamed” (angalia H hapo juu) mara 4 kwa siku, yaani ml 200 kwa siku, kwa siku zisizopungua
7. Mtoto anaweza kufurahia zaidi “artemisia ya sukari ya anamed“ (angalia K hapo juu). Mpe
kijiko cha chai kilichosawazishwa mara 4 kwa siku; yaani jumla ya vijiko 4 vya chai.
Kama mtoto hajitambui, jaribu yafuatayo: chukua quinine ya maji, au yeyusha vidonge vya
quinine (mg 30 za quinine kwa kilo moja ya uzito wa mwili kwa siku) katika ml 50 za maji,
gawanya dawa hii katika sehemu 4 au zaidi na umwinike mtoto kwa siku 1. Acha kumwinika
mgonwja mara tu apatapo fahamu, kisha mpe dawa inayotakiwa kupitia mdomoni.
Kama quinine haipatikani, unaweza kujaribu kumwinika kwa kutumia artemisia: Changanya ml
100 za maji yanayochemka katika gramu 2 za majani makavu, au gramu 10 za majani mabichi,
subiri kwa dakika 15, chuja, na acha ipoe. Tumia chai hii kuinika ikiwa imegawanywa katika
dozi 4 au zaidi katika siku 1. Fanya namna hii kwa siku 7, au hadi hapo mgonjwa atakapoweza
kunywa tena. Kwa wakati huu nunua dawa nyingine kwa sababu artemisia pekee inaweza
isitoshe kwa mtoto huyu.
Kwa kundi la umri huu, Artemisia annua inaweza pia kuchanganywa na proguanil au
cotrimoxazol.
Kama mgonjwa hajitambui, jaribu yafuatayo: Changanya ml 150 za maji yanayochemka kwenye
gramu 3 za majani makavu au gramu 15 za majani mabichi ya artemisia, subiri kwa angalau
dakika 15, chuja na uache ipoe. Ongeza vidonge vya quinine au quinine ya maji (mg 30 za
quinine kwa kila kilo ya uzito). Mwinike, dawa igawe katika dozi 4 au zaidi na itumike kwa siku
1. Endelea kumwinika kwa muda wa siku 7. Mara tu mgonjwa atakapoweza kunywa tena, mpe
dawa zote kwa njia ya mdomo.
Kwa kundi la umri huu, Artemisia annua inaweza pia kuchanganywa na proguanil,
cotrimoxazole au malarone.
Katika hili kundi la rika, Artemisia annua inaweza pia kuchanganywa na proguanil,
cotrimoxazol, malarone, au primaquin.
Kwa matatizo yafuatayo, unaweza kuamua kama unakunywa artemisia katika kiwango kikubwa
kwa siku cha gramu 5 au kipimo cha chini cha gramu 1.25.
Dozi kubwa: Changanya lita 1 ya maji yanayochemka katika gramu 5 za majani makavu, au
gramu 25 za majani mabichi, na kunywa katika siku 1. Majani makavu yaliyochekechwa ya
gramu 5 ni sawa na vijiko 4 vya chai.
Kipimo cha chini: Changanya ml. 200 (kikombe kikubwa 1) cha maji yanayochemka katika
gramu 1.25 za majani makavu, au gramu 6,25 za majani mabichi, na unywe katika siku 1. Kijiko
1 cha chai cha majani makavu yaliyochekechwa ni sawa na gramu 1,25.
Kuzuia Malaria
Washiriki wengi wa anamed katika nchi za Afrika walitambua kwamba wakinywa chai ya
artemisa anamed siku kwa siku wanapata malaria mara chache sana au kama wanapata, malaria
haina nguvu kama ilivyokuwa bila kutumia chai ya artemisia anamed.
Kwa sasa kampuni mbalimbali (k.mf. katika nchi za Burundi, Cameroon, Uganda) wanawashauri
wafanyakazi wao kutumia chai ya artemisia kwa ajili ya kuzuia malaria.
a) Kwa watalii kutoka Ulaya (wasio na kinga ya Malaria) wajaribu njia ifuatayo:
Mwaga kikombe 1 (ml 200) ya maji yanayochemka kwenye gramu 1,25 ya majani makavu ya
artemisia annua anamed (sawasawa ya kijiko 1 cha chai) na ipoe kwa angalau dakika 15. Chuja
na kunywa kikombe kizima mara moja. Usigawanye kikombe hiki – kwa sababu kwa njia hii
unahakikisha kuwa na kiasi cha artemisinin kwenye damu yako ambacho ni mara 4 zaidi kuliko
kiasi kinachohitajika kuua vidudu vya malaria. Watoto wanatakiwa kutumia kiasi kidogo zaidi –
kulingana na uzito wao. Wasioweza kutumia chai ya artemisia kutokana na uchungu wake
wanaweza kuponda majani yake na kuchanganya unga wake na yoghurt au peanutbutter au asali.
Anza kutumia njia hiyo siku unapofika katika nchi ya Afrika, endelea kutumia siku kwa siku na
endelea ukiwa umesharudi nyumbani kwa angalau wiki 3.
b) Kwa waliozaliwa au wanaoishi katika nchi za Tropiki (SEMI-IMMUNES) wanaweza kutumia
chai ya artemisia ya anamed mara 1 au mara 2 kwa wiki tu. Hii inaweza kupunguza malaria kwa
asilimia 50 %.
UKIMWI:
Huduma za kusaidia kuimarisha mfumo wa kinga ya mwili: Artemisinin imeishaidhinishwa
kutumika kama dawa ya kupunguza makali ya UKIMWI. Katika vituo kadhaa vya afya ambavyo
vinatumia madawa ya asili wagonjwa wa UKIMWI wanakunywa chai ya artemisia, katika dozi
ya juu au ya chini, kila siku ya maisha yao. Inapowezekana wanatumia pia chai ya mchaichai,
unga wa mlongelonge, vitunguu saumu kwa vingi au ute mzito wa msubili. Kwa taarifa zaidi juu
ya tiba ya UKIMWI/VVU kwa madawa ya asili, angalia toleo la anamed liitwalo “UKIMWI na
madawa ya asili”.
Kichocho:
Artemisinin hupunguza idadi ya vidudu vya kichocho. Jaribu kutumia dozi ile kubwa lakini pia
endelea kutumia chai hiyo kwa majuma 2 hadi 3. Ikiwezekana ongeza matibabu ya vidonge pia.
Tafadhali angalia matokeo ya tiba ya dawa hii katika maabara na ututumie matokeo yako.
Utafiti wa hivi karibuni ulionesha kwamba wanyama walioambukizwa na Kichocho na kutibiwa
kwa kutumia Artemeter, walionesha matokeo ya kupona, (Utafiti ulifanyika na Institute of
Parasitic Diseases, Shanghai, and the Swiss Tropical Institute, Basel pamoja na Ushirika wa
Afya Ulimwenguni (WHO).
Chikungunya na Dengue Fever: Tumia ile dose kubwa ya chai ya artemisa anamed kwa wiki 2.
Kutokana na maelezo tuliyoyapata, muda wa homa na kiasi cha maumivu kinapungua.
Homa, mafua ya kawaida:
Maambukizi yakitokea mara ya kwanza kunywa lita 3 za chai ya mchaichai kila siku. Kama joto
litaendelea au kama mafua au kikohozi kitaendelea basi kunywa lita 1 ya chai ya artemisia (dozi
kubwa) na lita 2 za chai ya mchaichai kila siku kwa siku 7 hadi 12.
Bawasiri: Hii ni kumbukumbu ya kwanza kabisa ya matumizi ya chai ya artemisia katika dawa
za jadi za ki-China. Kunywa lita 1 ya chai ya artemisia kila siku. Katika jimbo la Gamo Gofa
nchini Ethiopia watu wengi wanasumbuliwa na bawasiri sugu, na wamekuwa na mabadiliko
makubwa kwa kutumia tiba hii (kwa dozi kubwa – angalia hapo juu). Kwa bawasiri ya kawaida,
kunywa mara chache kikombe cha chai ya artemisia (dozi ya chini). Kwa matumizi ya nje pia
tumia artemisia ya mafuta (angalia sura ya 12).
Maambukizi ya macho:
Njia ya utengenezaji A: Watu wengi katika nchi za tropic hawaoni (Trachoma) kwa sababu
wakiwa watoto, wakisumbuliwa na inzi, hawakuwa na fedha za kutumia dawa. Njia
zinazoelezwa hapo chini ni kwa ajili ya dharula tu – wakati ambapo dawa ya macho hazipatikani.
Tahadhari: watu kutoka Ulaya mara nyingine wana allergy ya maua ya artemisia. Uhakikishe
kwamba hawana allergy na pia tumia dawa tu ambayo kwa uhakika haikutengenezwa kutokana
na maua.
Tayarisha chai ya artemisia kwa kuchemsha majani kwenye maji. Chemsha gramu 5 za majani
makavu katika kikombe 1 cha maji kwa dakika 5. Chuja kwa karatasi na uache ipoe. Weka
kitambaa safi cha pamba katika chai hii na ichemshe tena kwa muda mfupi. Ikiishapoa, weka
kitambaa hiki chenye dawa katika macho yako kwa dakika 5. Rudia tiba hii mara kadhaa kwa
siku. Tibu macho yako pia kwa ute mzito wa msubili. Kata jani la msubili kwa marefu kupitia
katikati na uguse jicho kwa kutumia ute huo. Kwa wakati huo huo kunywa chai ya A-3 (dozi ya
juu) iliyotengenezwa kwa kumwagia maji katika unga wa artemisia au majani mabichi
(infusion).
C. MATUMIZI MENGINE
Dawa ya mifugo:
Tulipata taarifa za mafanikio zilizotushangaza kutoka watu mbalimbali – mojawapo kuwa
matibabu ya saratani kwa mbwa. Kwa ujumla, baada ya kuvuna majani ya artemisia, matawi
yaliyobaki yanaweza kutumika na wanyama ili watafune kulingana na mahitaji yao. Artemisia
inatibu maambukizo ya wadudu (bacterial infections) na hata ugonjwa wa coccidiosis
unaosababisha kifo kwa wanyama.
Wanyama wengine wanaweza kupewa majani (mabichi au makavu) yaliyokatwakatwa na
kuwekwa kwenye chakula chao. Pendekezo ya dose kwa kuku, nguruwe, njiwa nk (badala ya
kutumia antibitic): gramu 10 za majani ya artemisia yaliyokaushwa kwenye kilo 1 ya chakula
chao. Watumie kwa siku 5 hadi 10.
Watafiti huko Romania waliponyesha kuku wao waliougua ugonjwa wa eimeriosis (ugonjwa
unaoathiri ngozi ya ndani ya matumbo) kwa kutumia gramu 15 za majani makavu ya artemisia
kwenye kilo 1 ya chakula chao.
Artemisia annua (sweet wormwood) pia inajulikana kwa kutibu minyoo na viroboto.
Viuatilifu vya kilimo: Wakulima katika nchi ya Tanzania waligundua kwamba wakiweka
mistari ya mahindi katikati ya mistari ya artemisia, mahindi yanapata madhara mchache zaidi
kutoka kwa wadudu na kwa hiyo hayahitaji dawa ya sumu ili kuua wadudu.
Kuzuia mbu: Ili kufukuza mbu weka miche ya artemisia au matawi ya artemisia kwenye
chombo cha maji ndani ya nyumba yako.
Nondo: Weka majani makavu ya artemisia yaliyofungwa kwenye kitambaa au kwenye mfuko
wa plastiki katikati ya nguo zako
Vinywaji: Kwa kutengeneza kinywaji ili kuepukana na matumizi ya soda, chemsha gramu 5 za
majani makavu au gramu 25 za majani mabichi kwenye lita 1 ya maji kwa dakika 10. Kwa kila
kikombe 1 cha chai hii ongeza vikombe 20 vya maji masafi na maji ya malimau 10. Tumia ikiwa
baridi sana.
9.2. Uoteshaji:
Mwarobaini unaoteshwa vizuri kutokana na mbegu zake. Chukua mbegu zilizotoka mtini –
zinaota kama zina umri usiozidi miezi 3. Ondoa maganda yake na kuweka kwenye magazeti
yaliyolowana na maji. Weka mahali penye joto na hakikisha magazeti yawe na unyevu wakati
wote. Baada ya wiki 1 ondoa magazeti na weka mbegu kwenye udongo wa mchanga kwenye trei
mahali penye mwanga, pasipo na jua la moja kwa moja. Baada ya majuma 2 zipandwe moja kwa
moja katika vyombo vya kukuzia vyenye udongo uliotengenezwa kwa udongo 50% na mboji
iliooza vizuri 50%. Kisha, baada ya miezi 3, zipandwe sehemu ya mwisho zitakapoishi wakati
wote.
Kwa kuotesha kwa vipandikizi, kata kitawi na ukiondolee majani kisha kichomeke kwenye
udongo wenye unyevu. Kwa kuotesha kwa mizizi, chimba kama meta 2 kutoka kwenye shina la
mti uliokomaa, na tafuta mzizi uliolala usawa wa ardhi ulio na unene wa kati ya sm 2 na 4. Ukate
katika urefu kama wa sm 20, na uchomeke sm 5 chini.
Mwarobaini inaweza kupandwa kwenye mteremko ya juu ya milima, ardhi isiyostawisha mazao
yoyote, karibu na barabara kwenye ardhi isiyo na kina cha udongo na yenye mawe na hata
kandokando ya bahari.
B. Tiba ya ngozi
Mwarobaini ni mzuri sana katika kutibu aina nyingi za magonjwa ya ngozi kama vile chunusi,
maambukizo ya mba, psoriasis, upele na eczema. Inaweza kutumika pia kutibu mzio.
Oga !: Kwa jadi, Wahindi walioga maji ya moto yenye majani ya mwarobaini.
Dawa ya mafuta:
- Dawa ya mwarobaini ya mafuta isiyo kali: Changanya gramu 10 za majani makavu
na gramu 100 za mafuta ya mboga, chemsha kwa saa 1 katika fukizo–maji, chuja na
kisha uchanganye na gramu 10 za nta ya nyuki iliyoyeyushwa.
- Dawa ya mwarobaini ya mafuta iliyo kali kiasi: Changanya gramu 10 za unga wa
mbegu kavu na gramu 100 za mafuta ya kula, chemsha kwa saa 1 katika fukizo-maji,
chuja na uongeze gramu 10 za nta ya nyuki iliyoyeyushwa.
- Dawa ya mwarobaini ya mafuta iliyo kali sana: Yeyusha gramu 10 za nta ya nyuki
katika ml 100 za mafuta ya mboga. Ikikaribia kupoa, ongeza ml 10 za mafuta ya
mwarobaini.
Dawa ya maji (tincture): Zamisha gramu 20 za majani makavu katika ml 100 za kileo
chenye 70% (Ethanol kwa matumizi ya nje, au kileo kilichotengenezwa kijijini). Baada
ya juma 1, chuja mchanganyiko huo. Ukitaka tu kuitumia, ndipo uchanganye kijiko 1 cha
chai cha tincture hii na kijiko 1 cha chai cha mafuta ya mboga na upake kwenye eneo
lililoathirika.
Baka la mba kwenye miguu (Athlete’s foot): Sugua majani kwenye eneo lililoathirika. Ama
tumia mchanganyiko wa tincture na mafuta.
Kutunza nywele: Chemsha majani katika maji na utumie hayo maji kuosha kichwa kwa
kuondoa tatizo la chawa na mba.
Vivimbe (warts): Paka mafuta ya mwarobaini kwenye ngozi moja kwa moja.
Majipu: Kama majipu hayana mdomo, tengeneza kibandiko cha dawa kwa kutumia majani na
uweke.
Majipu yenye mdomo, vidonda, na upele mbaya: Majani lazima yachemshwe kwa dakika 10
kwenye maji kidogo kabla hayajatengenezwa kama kibandiko cha dawa na kutumika.
Candida: Candida ni mba kama hamira ambayo wakati wote inapatikana kwenye ute wa ngozi
za ndani, lakini inaweza isizuiwe na kinga ya mwili hadi ikasababisha madonda mdomoni,
kwenye uke na kwenye ngozi. Changanya sehemu 1 ya mafuta ya mwarobaini na sehemu 9 za
vitu vifuatavyo na utumie:
- Kwa candida ya mdomoni: asali
- Kwa candida ya kwenye ukeni: Yoghurt au mafuta ya mboga.
- Kwa candida ya kwenye ngozi: Mafuta ya mboni au mafuta yoyote ya mboga.
Vidonda sugu vinavyokataa kupona: Vitibu kwa mafuta ya mwarobaini mara 2 kwa siku.
C. Malaria
Tengeneza chai yake kwa kumwaga lita 1 ya maji yanayotokota kwenye gramu 5 za majani
yaliyokaushwa (au gramu 10 kwa malaria kali zaidi.) Kunywa kikombe 1 mara 4 kwa siku.
Kunywa vinywaji vingine kwa wingi, hasa lita 2 za chai ya majani ya mchaichai. Soma sura ya 5
juu ya malaria. Chai ya aina hii inaweza pia kutumika kutibu surua na kuharisha.
Angalizo: Kama ilivyosemwa juu, matumizi ya muda mrefu ya mwarobaini yanaweza
kusababisha madhara ya ini.
Kwa kuzuia malaria, ongeza kiasi kidogo cha mafuta ya mwarobaini kwenye mafuta ya taa ndani
ya taa ili kufukuza mbu, na tafuna majani kadhaa kila juma ili kuongeza kinga ya mwili.
Vifaa vya kuhifadhi nafaka visivyoruhusu wadudu kuingia vinaweza pia kutengenezwa kwa
kutumia mchanganyiko wa majani ya mwarobaini, udongo wa mfinyanzi na majivu.
Nguo pia zinaweza kulindwa dhidi ya nondo kwa kuweka majani ya mwarobaini yaliyokaushwa
kwenye kibindo.
Majani ya mwarobaini (Melia azadarach (kushoto) na
Azadirachta indica (kulia): mimea hii miwili ina sifa za dawa
na kiuatilifu zinazofanana. Kwa matumizi ya ndani, walakini,
tunapendekeza Azadiracta indica kwa sababu umefanyiwa
uchunguzi wa kutosha.
B. Minyoo
Utomvu wa papai bichi mara nyingi unafaa kwa aina zote za minyoo ya tumbo. Osha kisu kwa
maji yanayotokota, osha papai bichi likiwa bado limening’inia mtini, na ulichanje mistari wima
kwa kisu. Kinga utomvu wake moja kwa moja kwenye kijiko cha chai au kikombe.
Angalizo: Utomvu hii ni hatari kwa macho.
Dawa hii inywewe asubuhi kabla ya kula chochote, pamoja na maji mengi pamoja na dawa ya
kusababisha kupata choo.
Unaweza kutumia vifuatavyo kama dawa ya kupata choo:
1. Kula maembe au mapapai yaliyoiva sana kwa wingi.
2. Mafuta ya mboni ya hospitalini.
3. Cassia Occidentalis au Cassia alata. Chemsha kijiko 1 cha chakula cha
majani makavu au magamba ya mizizi kwa dakika 10 katika lita 1 ya maji.
Kunywa lita nzima. Utaona matokeo yake kama baada ya masaa 8.
Tiba hii itolewe mara moja tu, lakini irudiwe baada ya juma 1 ili kuhakikisha kwamba minyoo
yote imeondolewa. Tiba inaweza kutolewa pia wakati mgonjwa anaharisha tayari.
Umri Kiasi
Miezi 6 – mwaka 1 ½ kijiko cha chai
Mwaka 1 – miaka 3 Kijiko cha chai 1
Miaka 4 – miaka 6 Vijiko vya chai 2
Miaka 7 – miaka 13 Vijiko vya chai 3
Miaka 14 – mtu mzima Vijiko vya chai 4
E. Kikohozi
Chimba mizizi michache ya mpapai (siyo mzizi mkuu). Osha vizuri, ikate vipande vipande na
uchemshe nusu ya kiganja katika lita 1 ya maji kwa dakika 15. Chuja.
Watu wazima wanywe chai hii katika siku 1 tu. Watoto wanywe kidogo kutokana na uzito wa
miili yao.
F. Tatizo la pumu
Vuta moshi wa majani ya mpapai! Kausha na usage majani machanga ya mpapai na uyavute
kwenye kiko au kama sigara – au choma majani haya karibu na kitanda chako na uvute mvuke
wake. Badala yake, kunywa chai iliyotengenezwa kutokana na kiganja kizima cha majani ya
mpapai au kiganja cha majani ya mziwaziwa (Euphorbia hirta.)
G. Kama sabuni:
Yasuguliwapo kwenye ngozi, pamoja na maji mengi, majani ya mpapai yanasafisha mwili kama
sabuni ya asili! Kwa jinsi hiyohiyo yanawezekana kutumika kufua nguo za rangi.
I. Malaria:
Changanya maji yanayotokota na kiganja 1 cha majani mabichi yaliyo safi. Acha itulie kwa
dakika 15 na uchuje. Kunywa kwa awamu kwa siku nzima. Kwa nyongeza, kunywa lita 2 za chai
ya mchaichai. Endeleza tiba hii kwa siku 7. Angalia sura ya 5.
11.2. Uoteshaji
Mti huu hukua haraka kutokana na kupandwa kwa kutumia mbegu au vipandikizi, hata kwenye
udongo dhaifu. Jinsi unavyokua, utakavyozidi kuupunguza usirefuke ndivyo utakavyotoa majani
mengi zaidi.
11.3. Vilivyomo
Kwa virutubisho: Majani ni chanzo bora cha vitamini A, B na C. Yana
madini, hasa calcium, chuma na phosphorus. Pia yana protini kwa wingi, na
yamekuwa na amino acidi muhimu kama aminu asidi inayotakiwa kwa afya
bora, ambayo haziwezi kujizalisha zenyewe. Majani mabichi yana calcium
mara 4 zaidi ya ile iliyomo kwenye maziwa na vitamini A mara 4 zaidi ya
iliyomo kwenye karoti – na hizi zimeongezeka kwenye unga wa mlonge.
Kwa dawa: Moringa Oleifera ina tabia ya kupambana na bacteria
(isothiocynates). Hii pia inazuia kukua kwa chembechembe za ki-saratani.
Kumbuka: Mbegu za mlongelonge zinaweza kutumika kwanza kwa kutoa mafuta yake.
Makapi yake ambayo yanaweza kukaushwa na kutunzwa yana uwezo ule ule wa
kusafisha maji kama mbegu ambazo hazijakamuliwa mafuta.
12.2.Zana zinazohitajika
- Mimea iliyokaushwa na kupondwa
- Tumia mafuta yoyote mazuri ya mboga, mfano mafuta ya shea, mafuta ya mchikichi,
mafuta ya alizeti, mafuta ya karanga n.k. - USITUMIE vaciline. Kama unatumia mafua
yaliyotengenezwa nyumbani, uhakikishe maji yote yameondolewa na wadudu wote
wamekufa. Chemsha kwanza mafuta haya (kwenye joto la nyuzi 100 ° C)
- Tumia nta ya nyuki au nta ya mshumaa. Uwe mwangalifu: Siyo mishumaa yote
imetengenezwa kwa nta.
12.3. Maandalizi
a) Uandaaji wa sehemu za mmea zinazohitajika.
Kata vizuri sehemu zinazohitajika. Kausha ndani ya siku 3 kwenye kitambaa safi. Kwenye nchi
za joto kaushia kivulini. Kwenye nchi za ubaridi, au mahali palipo na unyevu mwingi, kaushia
juani kabisa. Kama baada ya siku 3 majani yatakuwa hayajakauka hata kuweza kufikichika
mkononi, kaushia kwenye jiko la jua (solar), kwenye joto lisilozidi nyuzi 40ºC. Twanga vizuri ili
kutengeneza unga mzuri.
e) Andika vibandiko
Vitambulisho ni vya muhimu! Kwenye vitambulisho andika jina lako, jina la dawa ya mafuta,
tarehe ilipozalishwa na tarehe dawa itakapomaliza muda wake (kwa kawaida ni miaka 2).
Matumizi kwenye semina: Vipimo hivi vinatosha kujaza vikopo 35 vya mikanda ya
kamera.
Kwa hiyo jiwe jeusi, ni kitu muhimu katika kila sanduku la huduma ya kwanza kwenye eneo la
tropiki!
1. MSIMAMO WA KIKRISTO
Luka 6: 9 – 10 : Yesu amponya aliyepooza siku ya Sabato.
Wafilipi 2: 5 – 8 : Uwe na nia kama ya Yesu
I Wakorintho 13:1 – 13 : Jambo muhimu kabisa ni upendo.
Mathayo 18: 18 – 20 : Enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi
wangu.
2. PAMBANA NA KUZAGAA KWA MIFUGO
Mithali 12:10 : Mwenye haki hujali uhai wa wanyama wake.
Kutoka 22:5 : Mfugaji lazima alipe fidia ya hasara iliyosababishwa na
mifugo yake.
I Samwel 16:11 : Daudi alikuwa mchungaji wa kondoo.
Yeremia 23:1 : Wachungaji wabaya hutawanya kondoo.
B. “Waganga wa madawa ya asili” watatafuta kuweka watu na jamii nzima katika afya
nzuri kwa:
1) Kuweka njia za kinga kwa kijiji au wilaya.
2) Kuelimisha watu katika njia za kujikinga kiafya; mfano kutotumia sabuni zenye zebaki
(“mercury”).
3) Kushiriki kikamilifu katika kikundi cha dawa za asili cha wenyeji wa mahali anapoishi.
4) Kulinda mimea ya dawa.
5) Kujifunza majina ya kisayansi ya mimea inayotumika.
6) Kuanzisha bustani ya uzalishaji wa dawa na bustani ya maonyesho ya dawa pamoja na
mimea yenye lishe bora.
7) Kutumia chai za dawa kwa njia zilizoelekezwa (angalia “Dawa za asili katika nchi za joto
I” Sura 4:2).
8) Kutumia maelekezo mengine yaliyo salama kutengenezea dawa kama dawa za mafuta,
mafuta ya dawa, maji -chumvi (ORS), dawa za unga, jiwe jeusi n.k.
9) Kushughulika na ugonjwa mmoja tu.
10) Kutoa dozi zinazotakiwa.
11) Kutumia kipima joto.
12) Kushirikiana na hospitali kuwapeleka wagonjwa ambao huwezi kuwatibu au walio na
joto kali; au walio na hali mbaya sana.
13) Kukubali malipo yanayofaa kutoka kwa wagonjwa, kutokana na jinsi wawezavyo
kujipatia kipato.
14) Kufundisha wengine juu ya dawa za asili.
15) Kuwajali kwa upendo wagonjwa wa UKIMWI, na kutibu dalili na magonjwa
yanayohusiana na ugonjwa wa UKIMWI, ili waweze kuishi maisha marefu na mazuri.
Kwa kufuata mwongozo huu kila Mganga wa Asili anaweza kuwa mfanyakazi wa afya ya
msingi. Vivyo hivyo kwa kufuata hatua zilizotajwa chini ya namba 2 hapo juu, kila mfanyakazi
wa afya ya msingi anaweza kuwa Mganga wa asili.
anamed : Matoleo mbalimbali
Schwafweide 77, 71364, Winnenden, Germany.
e-mail kwa kuagiza: anamedhmh@yahoo.com
website: www.anamed.net
Kwa kiingereza:
105: Hirt/M’pia, “Natural Medicine in the Tropics I,” toleo la pili.
106: Kitabu hiki pamoja na kipeperushi cha rangi (403).
109: Hirt/Lindsey, “Natural Medicine II - Treatments” kKitabu cha maelezo ya semina.
113: Natural Medicine: III Seminar Leaders’ Resource kit.
114: Lindsey, “Making peace: Biblical principles.”
115: “Natural Medicine: IV AIDS and Natural Medicine.”
116: Hati “Four ULOG Solar ovens and one drier: Construction plans and uses.”
117: Hati: “Neem in medicine and agriculture.”
403: “Colour poster of 60 tropical medicinal plants 70×50cm.”
- Kipeperushi cha rangi cha mimea 60 ya madawa iliyo eneo la tropiki
70×50sm.
107: Lindsey/Hirt “Use water Hyacinth.”
201: Taarifa, “Be black, stay beautiful.”
204: Hati, “Malaria: Artemisia annua” pamoja na maelezo ya jinsi ya kulima.
GERMAN
101: Hirt /M’pia “Natürliche medizin inden tropen.”
102: Kitabu hiki pamoja na kipeperushi cha rangi (401).
401: Kipeperushi cha rangi, “Heilpflanzen in den Tropen 70×50cm.”
303: Taarifa za mbegu za mimea inayoponya: kununua, kutunza.
202: Hati “Malaria: Artemisia annua” pamoja na maelezo ya mwongozo wa jinsi ya
kulima.
KIFARANSA
103: Hirt/M’pia “La medecine Naturelle I”
104: Kitabu hiki pamoja na kipeperushi cha rangi (402).
112: “La Medecine Naturelle: II Traitements” Kitabu cha mwongozo wa semina, 40
pp.
118: “La Medicine Naturelle: III Guide du Formateur.”
402: Kipeperushi cha rangi, “Plantes medicinales tropicales” sm70×50
206: Taarifa “Sabuni za zebaki: Kashifa ya siku hizi.” (kwa kifaransa)
203: Hati “Malaria: “Artemisia annua” pamoja na maelezo ya jinsi ya kuilima.
KIHISPANIA
110: Hirt /M’Pia “Medicina Natural” 160 pp.
207: Taaifa: “Malaria” “Artemisia annua” pamoja na maelezo ya jinsi ya kuilima.
121: “Medicina Natural en el Tropica: Parte B”
KIRENO
120: Hirt/M’Pia “Reme’dios Naturais nos Tropicos : I.”
111: Hirt /M’Pia “Reme’dios Naturais nos Tropicos: II Tratamentos” kitabu cha
mwongozo wa semina.
205: Taarifa “Malaria: Artemisia annua” pamoja na maelezo ya jinsi ya kuilima.
405: Kipeperushi cha rangi cha mimea 60 ya madawa, sm70×50.”
KISWAHILI
123/ "Madawa ya Asili-1", Tome 1,
119/ "Dawa za Asili-2", Tome 2, Uzoefu (Seminars)
124/ "Ukimwi na Madawa ya Asili“ Tome 4, (AIDS and Natural Medicine
406/ Colour poster of 60 tropical med.plants (70x50cm), in Swahili,
453/ “Black is beautiful” 10 Posters DIN A3 about dangerous cosmetics, Swahili
ZANA NYINGINE
400: Karatasi kubwa nyeupe ya sm 70×50 yenye gamba jembamba pande zote kwa
kufundisha kwa marker-pen.
404: Kipeperushi cha rangi chenye mimea 60 ya madawa, bila maneno ya ufafanuzi zaidi; ina
gamba laini kwa ajili ya matumizi ya markers.
408: Mkusanyiko wa mbegu za kitropiki (Tayari kwa kuota).
409: Vikorokoro vya kuanzia ulimaji wa Artemisia vikiwa na mbegu 5,000.
412: Mbegu za artemisia, kifuko cha kujaza tena kwa ajili ya 409.
419: Mbegu za Moringa oleifera na maelezo ya kiingereza; na muhtasari kwa
kifaransa.
431: Vipandikizi vya Artemisia au miche (kutokana na upatikanaji) kwa ajili ya
uoteshaji.
411: Majani ya artemisia yaliyokaushwa kwa ajili ya matumizi ya kisayansi, 250g.
Picha ya nyuma kwenye kitabu: “Watu wa mataifa mbalimbali – kufuata mistari ya biblia –
wanasaidiana kuheshimu mimea ya dawa”. (Mchoro wa Gregor Müller, St Gallen,
Switzerland).